Ukitaka kuishi kwa furaha na amani: kwanza, punguza matarajio juu ya watu. Pili, wajibika zaidi kwa matatizo yako na mambo yahusuyo furaha yako. Huwezi kuangushwa wala kuumizwa na kitu usicho na matarajio nacho au mtu usiye na matarajio naye. ~Togolani Mavura.
"Furaha yako ni kero kwa wengine, mateso yako ni furaha kwa wengine. Furahi kwa sauti ndogo, teseka kwa sauti kubwa. Watakuvumilia ukiteseka kwa sauti kubwa lakini sio ukifurahi kwa sauti kubwa." ~Togolani Mavura.
"Sadaka huanzia moyoni na si mfukoni. Toa kwa sababu moyo wako umeguswa na si kwa sababu mfuko wako umefurika. Sadaka yako haitapimwa kwa kiasi bali kwa imani".~Togolani Mavura
"Kushinda si lazima mwingine ashindwe, kupata si lazima mwingine akose, kufurahi si lazima mwingine aumie.Kila mmoja hupata kilicho Kadri yake." ~Togolani Mavura.
"Ni vizuri kuwa na fedha na vitu vinavyonunuliwa na fedha,ni muhimu sana kutopoteza vile ambavyo fedha haiwezi kununua ambavyo ni imani,afya,upendo na utu." ~Togolani Mavura.
"Kipimo cha kujua sasa umekuwa mtu mzima ni pale ambapo idadi ya
wanaokulilia shida wewe inaongezeka wakati idadi ya wewe unaoweza kuwalilia shida inatoweka. Yakikufika pokea kwa moyo mkunjufu, yanakujaga na baraka zake." ~Togolani Mavura.
"Usipuuzie vijitabia vidogovidogo vya maudhi anavyovionesha mtu kwako maana ukweli wa mtu uko katika vijitabia vidogodogo vinavyomponyoka bila kutarajia na si katika mambo makubwa anayojinasibisha nayo." ~Togolani Mavura.
"Mwenyezi Mungu ameficha katika macho ya binadamu mambo 3, umri, rizki na kiama. Hatujui tutaishi miaka mingapi, hatujui rizki yetu ya kesho na hatujui mwisho wetu na maisha yetu akhera yatakuwaje. Hekima yake ni tuwe wanyenyekevu." ~Togolani Mavura.
"Watoto wote wanapatikana kwa kudra za Mwenyezi Mungu tu na wala si juhudi za wazazi. Hakuna wa ndani, nje, wala haramu. Mtoto ni mtoto tu. Wote wanastahili utu na kuthaminiwa. Walipatikanaje, hilo haliwahusu watoto na wala si tatizo Lao". ~Togolani Mavura.
"Usijihesabie umekuwa mtu mzima mpaka utakapoelewa kuwa maisha binafsi ya watu wengine na faragha zao hayakuhusu, wala imani zao na mitizamo yao hailazimiki kufanana na yako. Utu uzima ni hekima ya kuishi na watu usiofanana nao." ~Togolani Mavura.
"Ni heri utingwe na majukumu kuliko usiwe nayo. Majukumu hutuepusha na shari na mitihani mingi ya maisha na hutufungulia riziki. Usipotingwa nayo, utakuwa na muda mwingi wa kuhangaika na maisha ya wengine. Itakugharimu. Shukuru Mungu unayo". ~Togolani Mavura.
"Tunaamka kuhangaika tena sababu bado tuna chembe ya tumaini kuwa leo yaweza kuwa bora kushinda jana na hata tusipofanikiwa leo, pengine tutafanikiwa kesho. Katika maisha, poteza vyote lakini usipoteze matumaini. Ukipoteza matumaini, umepoteza sababu ya kuishi." ~Togolani Mavura
"Kuwapa maarifa wengine hakukupunguzii maarifa yako uliyonayo bali huyaongeza. Maarifa unayoyatoa kwa wengine yanaachia nafasi katika ubongo wako wa kuruhusu maarifa mapya. Usipoyatoa kwa wengine, hayo uliyonayo yanachakaa."
"Wanafiki hawakwepeki. Wamekuwapo na watakuwapo na wametajwa kwenye vitabu vya dini. Ukibahatika kuwajua, jikaushe. Mnafiki unayemjua anaweza kukusaidia kumjua mnafiki wako usiyemjua. Utafaidika zaidi ukijifunza kuishi kinafiki na wanafiki." ~Togolani Mavura
"Ukipata cheo mahala papya, watakaokulaki mapema ni wafitini na walalamishi. Hawa watakusimulia mabaya tu kuhusu watu waliopo badala ya masuala. Wema na wachapakazi utawafahamu baadae kwa kazi zao. Wasikilize kwa tahadhari kubwa." ~Togolani Mavura.
"Aliyebuni saa na kalenda naye kaumbwa na Mungu iweje basi subira yako kwa Mungu uifungamanishe na saa na kalenda aliyotengeneza mwanadamu." ~Togolani Mavura.
"Kila nyavu ina samaki wake. Nyavu ya kibua huvulii dagaa, vivyo hivyo ya jodari huvulii kibua.Utavua wale wanaotosha ukubwa wa nyavu zako. Sote tunakwenda kuvua bahari moja, tunarudi na samaki tofauti. Kabla ya kuona wivu kwa alichovua mwenzako, hangaika na aina ya nyavu yako".
"Wenye kufurahia maisha ni wale wanaodunduliza mafanikio madogo madogo katika kila hatua ya maisha yao huku wakiyaendea yale mafanikio makubwa kuliko wale wanaoyasubiri mafanikio makubwa sana mwishoni ambayo huenda yasitokee". ~Togolani Mavura.
"Kuna vyeo vyenye Madaraka, kuna vyeo vyenye Mamlaka na kuna vyeo vyenye Ushawishi tu. Usipojua mipaka ya madaraka, mamlaka na ushawishi utajikuta katika matatizo na lawama." ~Togolani Mavura.
"Vyote ni mali ya Mungu, akichukua chochote, Shukuru, hata kama ni mwili wako, basi akikuacha hai muombe asichukue ulimi tu ili uweze kulitaja na kulisifu jina lake."~Togolani Mavura.
"Watoto wa kwanza (first born) wanabebeshwa na kubeba mizigo mikubwa ya wajibu na lawama. Matarajio makubwa ya familia juu yao yanawabebesha wajibu, na wanaposhindwa kuyafikia matarajio hayo wanabebeshwa mzigo wa lawama. Mwenyezi Mungu awabariki na kuwawekea wepesi."
"Wako wanaonza maisha kwa kufyeka pori, wako wanaoanzia kwenye shamba lililotayarishwa, na wako wanaoanzia kwa kuvuna mazao yaliyokwishapandwa na wazazi. Wengine wao ndio baba wa mafanikio,wengine ni watoto wa mafanikio na wengine wajukuu wa mafanikio.Mchezo mmoja, ligi tofauti!"
Kesho ni ufunguo wa mlango wa uwezekano wa mambo yote maishani. Kama kesho ipo na ukijaaliwa kuwepo, basi na uwezekano wa lolote upo. Wewe usiache ombea kesho yako tu. ~Togolani Mavura.
"Heshimu chaguo la mtu. Kila mtu ana mtu wake, kila muonekano una mvuto wake, kila umbile lina tunu yake na kila hulka ina mwenziwe. Hakuna aliye mbaya kwa wote, mzuri kwa wote au mwenye kumfaa yoyote. Kila mtu na maradhi yake." ~Togolani Mavura.
"Tenga muda kwa ajili ya kutafakari na kujitathmini (meditation), na tenga muda kwa ajili ya kufunga (fast). Haya mawili hukuimarisha nafsi na kukupa unyenyekevu. Ndio siri ya mafanikio ya Mitume na Watu Bora." ~Togolani Mavura.
"Nafsi na roho yako ikisita usiipuuzie, wasiwasi ndio akili, usipuuzie ile sauti ndogo moyoni inayokukataza,yaweza kuwa salama na nusra yako." ~Togolani Mavura
"Hata kama unamjua mtu, ukikuta foleni panga foleni, ukiiruka unamuweka huyo unayemjua katika wakati mgumu dhidi ya walioko kwenye foleni. Mpe nafasi huyo unayemjua atafute njia bora ya kukusaidia isiyokwaza watu. Ukiondoka yeye atabaki nao". ~Togolani Mavura.
"Katika maisha, usijisahau na kufurahia sana kufanikiwa maana kufanikiwa ni tukio tu katika maisha, changamoto kubwa ni kuendelea kufanikiwa na kuishi maisha ya mafanikio." ~Togolani Mavura.
"Mbali ni kituo kabla ya mwisho. Wengi huchoka wakifika mbali. Hapo mbali ndipo jitihada na ndoto nyingi za wale wenye kukata tamaa zinapoishia. Wanaofanikiwa ni wenye ujasiri wa kupavuka hapo mbali. Mafanikio huwa yako mwisho". ~Togolani Mavura.
"Ukiona umeomba kwa Mwenyezi Mungu msaada na haupati majibu, jua kuwa hiyo shida bado iko ndani ya uwezo wako kuitatua. Ukimya wa Mwenyezi Mungu nao ni jibu." ~Togolani Mavura.
Kwa udhaifu wetu, tunatenda dhambi kila siku iwe kwa kuwaza, kwa kunena, kwa kutenda au kwa kutotimiza wajibu. Ili kufidia, tujitahidi kutimiza japo ibada moja na kutenda wema kwa mmoja kwa siku kila siku kusawazisha dhambi zetu. ~Togolani Mavura.
"Kwa kuwa kila kinachozaliwa hufa, basi hatukuzaliwa ili tufe, tumezaliwa ili tutimize wito wetu katika kipindi tunachojaliwa kuishi duniani." ~Togolani Mavura.
"Kifo si foleni ya umri kwamba aliyetangulia kuzaliwa atatangulia kufa.Jiandae wakati wote na ishi maisha yote uwezavyo katika kila siku unayojaliwa kuishi. Ahirisha kila kitu isipokuwa ibada. Leo ndio siku uliyonayo, kesho ni ahadi tu." ~Togolani Mavura.
"Usiache kumsaidia mtu kwa kudhani tu kwamba msaada wako mdogo hauwezi kutatua shida yake ya muda mrefu. Nafuu ya japo ya siku moja ni ahueni kubwa kwa mwenye shida maana shida haizoeleki bali inahimilika tu." ~Togolani Mavura
"Usiandike kitu mtandaoni kama hamna kesho, usiandike kama uko faraghani, daima kumbuka mitandao ya kijamii ni hadhara na wino wake haufutiki. Fikiri,tafakari kisha andika." Togolani Mavura.
"Kuna walioletwa duniani kuwa mbegu, kuna walioletwa kuwa mizizi, wengine kuwa mashina, na wengine kuwa matunda, wengine matawi ya kivuli, na wengine kuwa kuni. Tambua nafasi yako, wito wako na wakati wako. Ishi wito wako." ~Togolani Mavura.
"Ukiwa nacho watakusakama kuwa unaringa, usipokuwa nacho watakusakama kwa masimango. Maumivu ni madogo ukisakamwa kwa kuwa nacho kuliko kusakamwa na masimango ya kutokuwa nacho".~Togolani Mavura.
"Ukiwa kijana tambua umebeba dhamana na wajibu wa kizazi kizima. Ndio maana akikosea kijana mmoja lawama wanapewa vijana wote, Lakini akikosea Mzee mmoja lawama haiendi kwa wazee wote." ~Togolani Mavura
"Ukishindwa kuwa na utajiri wa mali na pesa basi hakikisha unakuwa na utajiri wa ndugu na marafiki wanaoweza kukufanyia yale ambayo pesa na mali vinaweza kukufanyia. Umasikini mkubwa ni kukosa vyote, yaani, pesa na mtandao." ~Togolani Mavura.
"Kwenye maisha mnaweza kuwa rika moja, mkafanya kazi pamoja, mkapambana pamoja ila kudra za Mungu ndio zitaamua yupi ayatangulie mafanikio na yupi awe wa mwisho kuyafikia." ~Togolani Mavura.
"Kwenye kuposa na kujadiliana mahari wanakwendaga wachache ila kwenye harusi wanakuja wengi. Ndivyo maisha yalivyo, utahangaika na wachache ukifanikiwa watakujalia wengi. Iko hivyo na itabaki kuwa hivyo. Kubaliana tu na
hali halisi." ~Togolani Mavura.
"Hakuna mwaka mrefu wala mfupi. Urefu au ufupi wake unategemeana na matukio unayokutana nayo, unayoyapitia na majukumu unayokabiliana nayo." ~Togolani Mavura.
"Si kila mnyama anawindwa kwa kukimbizwa, wengine wanategwa na wengine wananyatiwa. Ndivyo ilivyo pia katika maisha, si kila riziki inapatikana kwa kukimbizwa, riziki nyingine hutegwa, na nyingine zinanyatiwa." ~Togolani Mavura.
"Kila mtu atafanikiwa kwa uhakika na kikamilifu kupitia talanta na wito wake.Kwanza tambua talanta na wito wako na mengine yote yatajipa." ~Togolani Mavura.
"Kama hauko tayari kuelewa kwa usia, mawaidha, maapizo na makanyo, dunia inao watu wengi wa kutosha walio tayari kukuelewesha kwa maumivu na vitendo." ~Togolani Mavura.
"Usimsimange mwenye shida wala kumuadhibu ambaye tayari ameadhibiwa na maisha.Kama huwezi kumtua mzigo wake basi usimtwike zaidi. Lawama yake itakuwa kubwa kwako uliyemuongezea mzigo mdogo kuliko yule aliyembebesha mzigo mkubwa" ~Togolani Mavura.